Uhakiki
wa kazi za fasihi andishi
Riwaya:
TAKADINI
Mwandishi:
ben hanson
Wachapishaji:
mathew bookstore and stationaries
Utangulizi
Takadini ni riwaya ambayo imelenga
kuzifumbua macho jamii ambazo bado zinashikilia mila na desturi ambazo
zimepitwa na wakati. Riwaya hii imelenga kueleza namna ambayo mila na desturi
zinavyotumika kuwakandamiza baadhi ya watu katika jamii hasa wanawake na watu
wenye ulemavu mbalimbali.
Msanii amemtumia mhusika TAKADINI
kuwakilisha watu wenye ulemavu wa ngozi. Pia amemtumia Sekai kuwakilisha kundi
kubwa la wanawake wanaonyanyaswa na kukandamizwa na mila na desturi za jamii
mbalimbali.
Msanii anasisitiza kuwa kama baadhi ya
watu wataelimika na kuwa na msimamo thabiti katika kukemea mila hizi kandamizi
kama walivyofanya mzee Chivero, Shingai na Sekai, tatizo hili linaweza kupungua
au kuisha kabisa.
Maudhui
Dhamira
Msanii amejikita katika kueleza
kuhusiana na ukombozi wa kiutamaduni. Msanii anaonekana kusukumwa zaidi na
suala la jamii kukumbatia mila na desturi zilizopitwa na wakati. Mila hizi
zimefikia hatua ya kutishia uhai wa baadhi ya watu katika jamii. Hii
inathibitika pale ambapo baada ya sekai kujifungua mtoto ambaye ni zeruzeru,
mila zilieleza kuwa mtoto huyu anapaswa kuuawa lakini pia mama yake alipokataa
suala la mwanae kuuliwa nae alitishiwa kuuliwa kutokana na kubishana na mila na
desturi za jamii yake. Katika ukurasa wa 18 msanii anasema “......endapo
wataamua mtoto auawe hata wewe utauawa kwa sababu ya kupinga sheria za
kale.....”
Kauli hii inaonesha wazi namna ambavyo mila
na desturi zinavyotumika vibaya. Pamoja na yote haya lakini msanii
anatusisitiza kuwa kutafuta haki na usawa katika kumsaidia mtu hapana budi
kutekelezwa bila kujali hatari yoyote inayoweza kutokea mbele. Hili
linathibitishwa na sekai, kuwa pamoja na vitisho vya kuuawa aliamua kumsaidia
mwanae asiuliwe. Msanii anaeleza “.....mtoto huyu asiye na msaada alimtegemea
yeye, kama tu alitaka aishi. Katika kijiji hiki, kati ya watu wa makwati,
zeruzeru hakuwa na nafasi.....” (uk. 19).
Hapa msanii anatueleza kuwa ukombozi
huweza kuletwa kwa kuanzia ndani ya nafsi ya mtu kama alivyofanya sekai.
Pia katika kupambana na mila na desturi
kandamizi msanii amemtumia mhusika shingai ambaye alikataa utaratibu wa
kuchaguliwa mchumba na kuamua kuolewa na TAKADINI. Shingai anasema,
“....huyu ndiye mtu ninayetaka anioe.
Hakuna aliyeniuliza kama nampenda Nhamo. Wewe na baba mlikuwa na hamu ya
kuniozesha katika familia ya manyamombe hata matakwa yangu
hayakusikilizwa..........nimechagua. Nakuomba msamaa wako mama, unaweza kuniua
kama ukitaka, lakini katu kwa nhamo siendi.....”(uk.118).
Hapa msanii anatuonesha kuwa katika
kuleta ukombozi lazima uwe tayari kujitoa mhanga kama walivyofanya sekai na
shingai katika kuleta ukombozi wa kiutamaduni katika jamii zao. Juhudi zao zilizaa
matunda kwani hata watu wengine walikiri kuwa sekai na TAKADINI wameleta
mabadiliko makubwa sana katika jamii ile. Kati ya walioshudia mabadiliko yale
ni Tendai ambaye anasema. “.....mmebadilisha mabo mengi kijijini hapa. Kwa sasa
sifikirii kwamba kuna mtu yeyote atakayekuwa na moyo wa kuharibu watoto
wachanga masope au wenye ulemavu. Ahsante nyingi kwako TAKADINI na kwa baba
chivero......” (uk. ...)
Mapenzi
Msanii anazungumzia suala la mapenzi kwa
undani katika riwaya hii ambapo ametuonesha kuwa kuna mapenzi ya dhati na
mapenzi yasiyo ya dhati. Msanii anasisitiza kuwa mapenzi ya dhati ndiyo huweza
kujenga jamii bora na iliyoshikamana katika kuheshimu haki na uhuru baina ya
wanajamiikwani hujihisi kuwa wana undugu wa damu. Mapenzi ya dhati
yaliyooneshwa katika diwani hii ni baina
ya sekai na TAKADINI, mzee chivero na sekai, mzee chivero na TAKADINI. Sekai
kwa makwati, sekai na Pindai na shingai kwa TAKADINI. Mfano shingai katika kusisitiza penzi lake
kwa TAKADINI anasema “....huyu ndiye mtu ninayetaka anioe....unaweza kuniua
kama ukitaka.....”(uk. 118). Hapa msanii anatuonesha kuwa japo TAKADINI alikuwa
ni mlemavu wa ngozi pamoja na mguu bado shingai alimpenda na hata kuwa tayari
kufa kuliko kutenganishwa nae.
Mapenzi ya uongo yaliyooneshwa katika
riwaya hii nipamoja na yale ya makwati kwa sekai ambaye alimtuhumu sekai baada
ya kujifungua mtoto ambaye ni sope.
Mila
potofu
Mila potofu ni zile taratibu za jamii
fulani ambazo kwa namna moja au nyingine zinaweza kusababisha madhara kwa watu au
viumbe wengine katika jamii. Katika riwaya hii msanii amelizungumzia suala hili
kwa kina hasa baadhi ya jamii kuendeleza mila za kuwabagua watoto wenye ulemavu
wa ngozi (albino) au viungo vingine vya mawili. Katika jamii ya kina sekai
hapakutakiwa kuishi mtu mwenye ulemavu wa ngozi, lakini pia baada ya sekai
kuamua kutoroka kwenda katika kijiji cha Mtemi masasi bado kulikuwa watu
walioamini kuwa zeruzeru nilazima wauawe. Msanii anasema “.......mtoto lazima
auawe.....na mama yake pia, kama tu atakataa kutengana na mtoto wake” (uk. 35).
Mila nyingine potofu ni wazazi
kawachagulia watoto wao wachumba. Hili ni suala ambalo lipo katika jamii zetu.
Hali hii inathibitishwa na tendai ambaye alilazimishwa kuolewa na Mtemi masasi,
katika ukurasa wa 47anasema.
“....namchukulia kama baba yangu badala ya mume wangu...” Hapa tendai
anaeleza namna anavyokumbana na changamoto katika ndoa yake ambayo
alilazimishwa kuwepo.
Suala la kuchagulia watoto wachumba
halina budi kusitishwa kwani hutengeneza familia zisizo na furaha na maelewano.
Ujasiri
Ujasiri ni ile hali ya kujiamini katika kulikabili
jambo fulani. Msanii anasisitiza kuwa
tunapaswa kuwa wajasiri ili kuweza kufanikisha jambo katika maisha. Msanii
amemtumia sekai kuonesha namna ujasiri unavyoweza kufanikisha mambo kwani sekai
asingekuwa jasiri angeweza kumpoteza mtoto wake wa pekee.
Pia shingai ameonesha ujasiri mkubwa
katika kujikomboa katika makucha ya mila kandamizi za kulazimishwa kuolewa na
mtu asiyempenda.
Ujasiri mwingine ni ule uliooneshwa na
mzee chivero kuwa pamoja na kujua watu wa kijiji chake hawataki zeruzeru aishi,
yeye alikubali kumpokea sekai na mwanae TAKADINI japo alikuwa sope.
Ndoa
za mitara
Hizi ni ndoa zinazohusisha mke au mume
zaidi ya mmoja. Katika riwaya hii msanii anaeleza kuwa ndoa hizi zimekuwa ni
chanzo cha kutokuelewana na kuzua mitafaruku katika familia nyingi. Msanii
amemtumia makwati ambaye alikuwa na wake
watatu ambao ni sekai, Dadirai na Rumbidzai. Ndoa hii haikuwa na maelewano
mazuri kwani makwati alionekana kumpenda zaidi sekai kuliko dadirai na Rumbidzai,
hali iliyoleta kutokuelewana baina yao. Msanii anasema “....baada ya kuonja
vyakula hivyo, aliishia kula chakula kilicholetwa na sekai....tukio hili
lilimhuzunisha sana Rumbidzai ambaye alitaka apendwe zaidi....”(uk.2).
Pia ndoa ya Mtemi Masasa ilionekana
kutokuwa na maelewano kwani tendai ambaye alikuwa ni mke mdogo alionewa na
kunyanyaswa na wake wakubwa ambao ni kama mama zake.
Suala la ndoa za mitara linapaswa
kuangaliwa kwa undani kwani pakikosekana uadilifu huweza kuleta ugomvi
utakaopelekea kuvunjika kwa ndoa hiyo au migogoro isiyo na kikomo.
Umoja
na mshikamano
Umoja ni ile hali ya kuwa pamoja, mshikamano
ni ile hali ya kushirikiana kinguvu na kifikra katika kutimiza azma fulani.
Mwandishi anatuonesha kuwa ili kuweza kutatua matatizo makubwa yanayoikumba
jamii hatuna budi kushikamana kwa umoja wetu. Katika riwaya hii mshikamano
mzuri baina ya mzee chivero, sekai, Mtemi masasi, na tendai umewawezesha kuokoa
maisha ya TAKADINI.
Nafasi
ya mwanamke katika jamii
Katika
riwaya hii msanii amemchora mwanamke
katika sura tofauti tofauti. Msanii anamtazama mwanamke kama kiumbe jasiri na
mwenye maamuzi magumu katika kutetea lile analolitaka. Hii inathibitika
kwa kumtazama sekai ambaye aliamua
kuhatarisha maisha yake kwa ajili ya kuokoa maisha ya TAKADINI. Pia msanii
amemtumia shingai kuonesha ujasiri wa mwanamke katika kusimamia lile alitakalo.
Shingai anasema, “huyu ndiye mtu ninayemtaka....unaweza kuniua kama ukitaka...”
(uk. 116).
Mlezi wa familia, mwandishi anamchora
mwanamke kama mlezi wa familia hasa watoto. Hili linathibitika kwa kumuangalia sekai
ambaye alimlea TAKADINI mpaka alipokua mkubwa na kupata mke. Pia Mashingai
alimzaa na kumlea shingai mpaka alipoolewa na TAKADINI. Hii inathibitisha kuwa
kazi ya kulea aliachiwa mwanamke pekee. Baba shingai anasema kumwambia mkewe, “hukumfundisha mwanao maana ya tendo
hillo wewe?” (uk. 96). Kauli hii inathibitisha kuwa wanaume hawakuwa na jukumu
la kulea watoto wao bali waliwaachia wanawake pekee.
Mwanamapinduzi, sekai na shingai
wameonesha kuwa mwanamke ni mwanamapinduzi kwani waliweza kubadili mioyo ya
watu katika mila na desturi zao. Sekai ameweza kuleta mapinduzi ya kiutamaduni
tena akiwa uhamishoni. Tendai anasema, “...sasa sifikirii kwamba kuna mtu
yeyote atakayekuwa na moyo wa kuharibu watoto wachanga, masope au wenye ulemavu....”
(uk. )
Shingai pia alionesha mapinduzi kwa
kukataa kuolewa na nhamo kama alivyochaguliwa na baba yake na kuamua kuolewa na
TAKADINI ambaye ni sope.
Kwa upande wa pili msanii amemchora
mwanamke kama kiumbe dhaifu asiye na maamuzi wala kuweza kuchangia mawazo yake
katika jamii. Hii inaonekana katika baraza la Mtemi masasi ambapo wazee wote wa
baraza walikuwa ni wanaume pekee.
Dhamira nyingine zilizojadiliwa katika
riwaya hii nipamoja na..............................
Migogoro
Riwaya hii imesheheni migogoro mingi
sana ikiwemo migogoro ya nafsi, migogoro ya mtu na mtu na hata migogoro ya
kijamii. Baadhi ya migogoro hiyo ni pamoja na;
Mgogoro baina ya makwati na sekai, mgogoro
huu ulitokea baada ya sekai kujifungua mtoto ambaye ni sope. Hali hii ilimfanya
makwati kumchukia sekai hali iliyopelekea sekai kutoroka ili kunusuru maisha ya
mwanae.
Mgogoro wa nafsi wa sekai mara baada ya
kukaa muda mrefu bila ya kupata mtoto, mgogoro huu ulitokea hasa mara baada ya
wake wenzake hasa dadirai na Rumbidzai kumsema vibaya juu ya hali hiyo ya
kutopata mtoto. Mgogoro huu ulisuluhishwa mara baada ya sekai kupata ujauzito wa
TAKADINI.
Mgogoro baina ya shingai na wazazi wake,
mgogoro huu ulitokana na shingai kukataa kuolewa na nhamo ambaye ndiye alikuwa
chaguo la wazazi wake na kuamua kuolewa na TAKADINI. Suluhisho la mgogoro huu
ni baada ya shingai kutoroka na kwenda kulala na TAKADINI hatimae akapata
ujauzito.
Mgogoro baina ya TAKADINI na nhamo, mgogoro
huu ulitokana na hali ya nhamo kupenda kumbagua TAKADINI na hata kumpiga pasi
na sababu yoyote. Migogoro huu haukupatiwa ufumbuzi hadi mwisho wa riwaya.
Mgogoro wa nafsi wa TAKADINI, mgogorohuu
unaonekana katika ukurasa wa 123 na 124 ambapo TAKADINI alikuwa anaweza ni kitu
gani kitatokea kama mtoto atakayezaliwa na shingai atakuwa sope kama yeye. Mgogoro
huu unasuluhishwa mara baada ya shingai kujifungua mtoto asiye na ulemavu wa
ngozi.
Migogoro mingine iliyojitokeza katika
riwaya hii ni pamoja na,
Mgogoro wa nafsi wa tendai mara baada ya
kuolewa na Mtemi masasi ambaye alikuwa na umri sawa na baba yake.
Mgogoro baina ya tendai na wake wenzake
ambao walimchukulia kama mtoto.
Mgogoro baina ya chido na shingai
kutokana na chido kuwa na wivu wa kimapenzi juu ya nhamo.
Mgogoro baina ya amai shingai na
nhariswa baada ya shingai kutoroka na kwenda kulala kwa TAKADINI.
Ujumbe
Jamii inapaswa kuachana na mila potofu
zinazopelekea unyanyasaji kwa baadhi ya makundi ya watu katika jamii kama vile
walemavu nawanawake.
Suala la ndoa na kuchagua mchumba
halipaswi kuingiliwa kwani ni maamuzi ya watu wawili waliopendana.
Msimamo, ujasiri, umoja na mshikamano ni
mambo muhimu sana katika kutafuta ukombozi wa kiutamaduni
Walemavu wana haki ya kuishi sawa na
watu wengine wasio walemavu.
Malezi ya watoto yanapaswa kusimamiwa na
wazazi wote wawili na si kumuachia mama pekee.
Wanawake wanaweza kufanya mambo makubwa
katika jamii hivyo wapewe nafasi ya kushiriki katika maamuzi.
Falsafa
Mwandishi anaonekana kuamini kuwa
binadamu wote ni sawa hata kama wana utofauti kimaumbile. Na kila binadamu ana
haki ya kuishi. Au
Mwandishi anaamini kuwa misingi ya haki
na usawa haina budi kuheshimiwa kwa kila binadamu bila kujali maumbile wala
jinsia yake.
Mtazamo
Mwandishi anautazama ulimwengu katika
jicho la kiuyakinifu ambapo anaona kuwa
matatizo yanayoikabili jamii yanaweza kutatuliwa endapo jamii itafuata misingi
ya haki na usawa kwa binadamu wote bila kubagua maumbile au jinsia.
Msimamo
Msimamo wa mwandishi ni kuwa, ili jamii
iweze kuondokana na matatizo mbalimbali hasa ya kiutamaduni nilazima ifuate
misingi ya haki na usawa kwa watu wote pasi na kubagua jinsia au maumbile.
Maoni
Chapisha Maoni